Sunday, November 18, 2012

Mjini Moshi: Wizi wa kuvunja vioo kwa kemikali watikisa



WIZI wa vitu mbalimbali kwenye magari madogo ya kifahari unaofanywa na watu wasiojulikana wanaovunja vioo vya magari kwa kutumia kemikali, umeanza kuutikisa mji wa Moshi.
Hata hivyo habari za uhakika zilizopatikana jana na kuthibitishwa na polisi zilisema wengi wa waliobiwa kwa njia hiyo hawatoi taarifa polisi japo matukio hayo yanaongezeka.
Watu wanaoendesha vitendo hivyo kwenye maegesho ya magari wanadaiwa kumwaga kemikali kama mafuta ya nywele za wanawake aina ya Curl ambayo hupasua kioo na kukiacha kama chengachenga.
Kikundi hicho kinadaiwa kulenga zaidi vifaa vya thamani kama kompyuta mpakato(Laptop),Kamera, fedha taslimu, simu za mikononi na pochi za wanawake ambazo kwa sehemu kubwa huwa na vito vya thamani na fedha.
Mthamini wa Halmashauri ya Manispaa ya Moshi,Hugo Michael ni mmoja wa waathirika wa tukio hilo ambaye alisema, binafsi aliibiwa mfuko uliokuwa na Laptop, Kamera na nyaraka mbalimbali za ofisi.
Alisema Jumatatu iliyopita aliegesha gari eneo la maegesho ya hospitali ya Rufaa ya KCMC na kwenda kumuona mgonjwa lakini aliporejea alikuta kioo cha gari yake kimepakwa mafuta na kusambaratika.
Mhandisi wa mradi mkubwa wa jengo la kibiashara la mfuko wa Hifadhi ya Jamii (NSSF) karibu na Halmashauri naye alikumbwa na tukio kama hilo na kuibiwa Laptop na nyaraka mbalimbali.
Mbali na wizi huo ,eneo la Soko la Mbuyuni, nako kumeibuka wimbi la wizi wa vitu mbalimbali kwenye magari yanayoegeshwa eneo hilo ambapo wezi hao hufungua milango na vioo vya magari.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kilimanjaro, Robert Boaz alisema matukio ya wizi wa kutumia kemikali bado hayajamfikia lakini ya wizi katika soko la Mbuyuni wana taarifa nayo na wanaendelea na uchunguzi.
Alisema polisi wamefanikiwa kukamata watuhumiwa wachache wanaodaiwa kuhusika na wizi huo lakini wanashindwa kuwafikisha mahakamani kwa kukosa ushirikiano kutoka kwa wanaoibiwa

No comments:

Post a Comment

sikiliza ngoma zinazo kamata kwa sasa

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...