Monday, January 28, 2013

LOWASSA ANUSURIKA KIFO BAADA YA GARI LAKE KUPATA AJALI MKOANI MOROGORO

 
Waziri Mkuu aliyejiuzulu, Edward Lowassa. 

WAZIRI Mkuu wa zamani, Edward Lowassa amenusurika kifo baada ya gari lake alilokuwa akisafiria kutoka jijini Dar es Salaam kwenda mkoani Morogoro, kupata ajali.

Habari zilizolifikia gazeti hili jana zilieleza kuwa Lowassa alipata ajali hiyo jana saa 2:00 asubuhi baada ya gari lake hilo kugongwa na basi la Moro Best eneo la Bwawani mkoani humo.

Kwa mujibu wa habari hizo ajali hiyo ilitokea baada ya basi la Moro Best lililokuwa likitokea Morogoro kuelekea Dar es Salaam, kujaribu kuyapita mabasi kadhaa na kukutana na gari la Lowassa kisha kuligonga ubavuni.

Hata hivyo, katika ajali hiyo hakuna aliyejeruhiwa na Lowassa ambaye ni Mbunge wa Monduli, aliendelea na msafara yake.

Lowassa alikuwa anaelekea Morogoro ambako pamoja na mambo mengine, alishiriki harambee ya ujenzi wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri (KKKT), Kilakala.
Akizungumzia ajali hiyo kabla ya kufanyika harambee hiyo, Lowassa  aliwaeleza waumini kuwa kunusurika kwake katika ajali hiyo ni kwa neema za Mungu tu.

“Mkono wa Mungu ni mkubwa, bila ya hivyo  simulizi zingekuwa nyingine juu yangu. Wakati nilipoliona basi likiwa linakuja upande wetu kutugonga, ulinijia wimbo mmoja unaosema ‘’Hivi haya yote ya nini, ni huruma tu,’’ alisema Lowassa.

Akizungumzia tukio hilo Mkuu wa Usalama Barabarani (RTO), Mkoa wa Morogoro, Leonard Gindo alisema taarifa za tukio hilo walizisikia na kuamua kufika eneo la ajali na kukuta vioo vilivyopasuka bila magari kuwepo.

“Hakuna taarifa iliyoripotiwa, lakini tukio hilo lilitokea na kwamba tulifika eneo la tukio na kukuta vioo tu. Inaelezwa kilichotokea ni basi la Moro Best kujaribu kulipita basi lingine na ghafla gari la Lowassa nalo lilikuwa linakuja kwa mbele,” alisema Gindo.
Alisema kuwa taarifa walizozipata ni kuwa magari yote yaliendelea na safari zake baada ya tukio hilo.

“Inasemekana basi la Moro Best liliendelea na safari yake na Lowassa naye aliendelea na safari yake ila vioo tulivyovikuta hatujajua ni vya gari gani,” alisema Gindo.

Kuhusu harambee
Katika harambee hiyo, Lowassa alifanikiwa kuchangisha zaidi ya Sh48 milioni, fedha ambayo ndiyo waliyopanga kuikusanya.

Lowassa alisema yeye na marafiki zake, wanatoa kiasi cha Sh18 milioni ili kuweza kufanikisha shughuli za kanisa hilo.

Alisema anaona faraja kutumia kiasi kikubwa cha fedha zake makanisani na angependa wanaohoji mkakati wake huo kuelewa hivyo.

“Watu wanahoji kwa nini natumia fedha zangu kwenye makanisa, mimi nina Mungu na ninapata faraja kufanya hivi,” alisema Lowassa na kuongeza; Ninachofanya ni kazi ya Mungu.”
Lowassa amekuwa akishiriki katika harambee za ujenzi na shughuli  mbalimbali za makanisa nchini tangu alipokuwa Waziri Mkuu.

Imeandikwa na Boniface Meena,Dar, Venance George na Lilian Lucas, Morogoro

HALI TETE MTWARA; SABA WAUAWA KATIKA VURUGU MASASI,NYUMBA YA ANNA ABDALLA,MARIAM KASEMBE ZACHOMWA MOTO,MMOJA AUAWA ULANGA

 
Wakazi wa mji mdogo wa Dumila Wilaya ya Kilosa mkoani Morogoro  wakiwakimbia askari wa Kikosi cha Kutuliza Ghasia (FFU)  katika barabara ya Dodoma-Morogoro juzi. Picha na Juma Mtanda 

WATU wanane wameuawa na wengine kumi na moja kujeruhiwa kutokana na vurugu zilizizotokea jana mkoani Mtwara na Itete wilayani Ulanga, mkoani Mororgoro.
Muuguzi wa zamu katika Hospitali ya Wilaya ya Masasi, Mkomaindo, Amima Simbo alithibitisha vifo vya watu saba waliofikishwa hospitalini hapo.
Kwa mujibu wa muuguzi huyo, maiti zilizopokelewa hospitalini hapo zilionekana zikiwa na matundu yanayodhaniwa kuwa ni ya risasi, baadhi yao kichwani, begani, viunoni na tumboni.
Aidha majeruhi waliofikishwa hospitalini hapo pia walikuwa na majeraha mbalimbali ikiwamo ya risari.
Habari zaidi zinaeleza kuwa vurugu hizo zilizuka baada ya kundi la waandamaji, wengi wakiwa vijana waendesha pikipiki maarufu kama bodaboda waliokuwa wakipinga mwenzao kukamatwa na kutaka kuvamia Kituo cha Polisi ili kumwokoa.
Vurugu hizo ziliendelea kuutikisa Mkoa wa Mtwara kwa siku ya pili mfululizo na kuutikisa Mkoa wa Mtwara, baada ya vurugu nyingine kuibuka wilayani Masasi jana.
Habari zinasema mbali na vifo na majeruhi, nyumba za wabunge wawili wa wilaya hiyo zimechomwa moto, ambapo pia magari, trekta, Ofisi za CCM Wilaya na Ofisi ya Mkurugenzi wa Wilaya ziliharibiwa kwa kuchomwa moto.
Wabunge ambao nyumba zao zimemwa moto ni Mariam Kasembe wa Masasi Mjini na Anna Abdallah Mbunge wa Viti Maalumu wilayani humo.
Juzi vurugu hizo zilitokea katika Mikoa ya Morogoro kati ya wakulima na wafugaji na kusababisha kifo cha mtu mmoja wakati mkoani Mtwara wananchi  wa eneo la Chikongola waliizingira nyumba ya diwani wa Kata ya Mikindani, Mohamedi Chehako kwa madai ya kuwahifadhi wachawi ndani ya nyumba yake.
Katika vurugu hizo polisi walilazimika kutumia silaha yakiwamo mabomu ya machozi ili kupoza hali ya hewa, ambapo nyumba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), Hawa Ghasia ilichomwa moto.
Akizungumza na Mwananchi Jumapili kuhusu vurugu hizo, Mbunge wa Masasi Mjini, Mariam Kasembe alisema kuwa nyumba yake iliyoko Masasi mjini imechomwa moto na kuteketea kabisa, huku mali zikiibwa na kwamba familia yake sasa haina makazi.
Aliongeza kwamba mbali na uharibifu, vurugu hizo zimesababisha pia mama yake mzazi kukimbia na mpaka sasa hajulikani alipo.
“Wamechoma trekta na gari lililokuwepo nyumbani kwangu, watoto wangu na mume wangu walipoona hali hiyo wakakimbia,” alisema Kasembe akieleza kuwa hawezi kuthibitisha chanzo cha vurugu hizo, lakini anahisi kuwa zinatokana na mgogoro wa gesi.
Alifafanua kwamba watu hao walifanya uharibifu huo baada ya kupanga njama huku wengine wakiwa wamekizingira Kituo cha Polisi, ili kuwazuia wasiende kuisaidia familia yake.
“Ofisi ya Bunge ilitaka kunisafirisha ili nikaangalie hali ilivyo, lakini wapigakura wangu na ndugu wameniambia nisiende ili kulinda usalama wangu,” alisema.
Naye Mbunge wa Viti Maalum (CCM), Anna Abdalla alisema nyumba yake iliyopo eneo la Masasi mjini imechomwa moto katika vurugu zilizotokea jana.
“Ni kweli nyumba yangu nimesikia imechomwa moto, lakini sijui kinachoendelea,” alisema.
Mkazi wa Kijiji cha Chikunja, alipozaliwa Kasembe, Anna Martin aliliambia gazeti hili kuwa kundi jingine la vijana lipo katika harakati za kutaka kuichoma nyumba ya mbunge huyo, hali iliyosababisha wanafamilia wa mbunge huyo kutoka nje.
Shuhuda mwingine wa tukio hilo, Idi Mkwachu, ambaye ni Mkandarasi wa Wilaya hiyo alisema kuwa vurugu hizo zilianza saa mbili asubuhi jana, ambapo kundi la watu lililokuwa likizunguka mitaani lilikuwa  likiimba nyimbo za kuitaka Serikali ilipatie ufumbuzi suala la gesi.
Mkwachu alisema kuwa suala la gesi limezua uadui mkubwa kati ya wananchi na Serikali huku akidai kuwa kuna siri imebainika kuwa wabunge wanaoshinikiza gesi itoke Mtwara, wamepewa mamilioni ya fedha na Serikali.
“Kwa mfano gridi ya taifa ingeanzia Mtwara ingekuwa ni karibu zaidi kuliko gridi hiyo kujengwa katika eneo jingine. Mbona  kujenga bomba ni gharama kuliko gridi hiyo?,” alisema Mkwachu.
Alisema kwamba Serikali inavyochukua muda mrefu kutoa suluhu ya mgogoro huo, inajipalia makaa kwa sababu mikoa ya Mtwara na Lindi imebobea katika umaskini kwa miaka mingi.
Mkwachu alisema kuwa hadi kufikia jana saa kumi jioni, baadhi ya majengo yalikuwa yakiendelea kuteketea kwa moto, huku askari kutoka Nanyumbu na Nachingwea wakiletwa ili kusaidia kutuliza ghasia hizo.
Maaskofu watoa tamko
Wakati hayo yakiendelea, Baraza  la Maaskofu wa Makanisa ya Kipentekoste (PCT) Mkoani Mtwara, limetoa tamko likiitaka  Serikali isitishe mpango wake wa kusafirisha  gesi  kutoka Kijiji cha Msimbati mkoani humo, kwenda Kinyerezi Dar es Salaam.
Tamko hilo limetolewa jana na Mwenyekiti wa Baraza hilo, Charles Chilumba walipozungumza na waandishi wa habari katika klabu ya waandishi wa habari Mtwara (MTPC), iliyopo mjini humo.
Chilumba alisema kuwa Serikali inatakiwa kuwa sikivu na kusikia kilio cha wananchi wa Mikoa ya Kusini  ya Lindi na Mtwara, ambako vyanzo vya uchumi wa gesi vipo ili kutekeleza madai yao.
Alisema kuwa, viwanda vya mbolea, plastic na saruji ambavyo viliahidiwa kujengwa, vijengwe sasa na zisiwe propaganda za kisiasa kutoka kwa viongozi wa Serikali, ili  kuondoa dhana iliyokuwapo miaka ya nyuma kuwa kusini ni  ukanda wa vita, hivyo hakuna sababu ya kuendelezwa.
“Serikali isisikilize wabunge wadanganyifu, ambao hawana makubaliano na wananchi katika majimbo wanayotoka, ambao huchochea mgogoro huu kwa lengo lao na masilahi yao binafsi,”alisema Chilumba.
”Inabidi wawaombe radhi bila masharti kwani semi zao  zinaleta chuki, uhasama, utengano katika nchi na kusababisha nchi isitawalike. Serikali ya CCM itekeleze Ilani ya Uchaguzi ya mwaka 2010 Ibara ya 63 kifungu H na K,”alisema.
Viongozi wa dini hao wameomba Mungu awape hekima viongozi wa  Serikali kwa kuwa wamepewa dhamana na Mungu kuliongoza taifa kwa umahiri, wakionya kuwa ukaidi wa wenye fitina utawaangamiza.
Alipotafutwa msemaji wa Jeshi laPolisi nchini, Advera Senso alisema kuwa hawezi kuzungumzia suala hilo na kuomba atafutwa Kamanda wa Polisi mkoani Mtwara, Maria Nzuki.
“Sawa lakini, naomba umtafute Kamanda wa Polisi wa Mtwara yeye ndiye ataweza kukujibu unachokiuliza,” alisema Senso.
Hata hivyo gazeti hili lilimtafuta Nzuki bila mafanikio kwani simu yake ya mkononi ilikuwa imezimwa.
Naye Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Pereira Ame Silima alipotafutwa alisema kuwa yeye siyo msemaji.
“Mimi siyo msemaji wa masuala hayo, mtafute Waziri (Emmanuel Nchimbi) yupo atazungumzia hilo,” alisema Silima.
Waziri Nchimbi naye kama ilivyokuwa kwa Kamanda Njiku, simu yake ya mkononi jana ilikuwa haipatikani.
Morogoro
Mkoani Morogoro mtu mmoja anayeaminika kuwa ni mfugaji katika Wilaya ya Itete, mkoani Morogoro ameuawa kwa kupigwa risasi na polisi baada ya kundi kubwa la wafugaji kuvamia viongozi wa halmashauri waliokamata mifugo yao kwa madai ya kulisha maeneo yaliyozuiwa.
Tukio hilo limetokea jana asubuhi baada ya viongozi wa eneo la Itete wilayani Ulanga, kupata taarifa kuwa kuna makundi ya mifugo yaliyokuwa yakilishwa ndani ya hifadhi ya ardhi oevu, ambayo Serikali imepiga marufuku kulisha mifugo.
Kwa mujibu wa ofisa mmoja aliyekuwapo kwenye operesheni ya kukamata mifugo hiyo na ambaye hakupenda jina lake liandikwe gazetini, alisema kundi hilo kubwa la wafugaji wakiwa na silaha za jadi waliwavamia na kuanza kuwashambulia kwa lengo la kuchukua mifugo yao iliyokuwa imekamatwa.
Alisema kwamba viongozi hao wa halmashauri walipewa taarifa ya kuwepo kwa mifugo hiyo katika eneo hilo na walipofika waliikuta mifugo hiyo na kuamua kuichukua kisha kuipeleka kwenye makambi yaliyotengwa kuhifadhi mifugo wilayani hapo.
“Baada ya kuchukua mifugo ile, wafugaji walipata taarifa kuwa tumeikamata mifugo yao, ndipo walipojikusanya na kutuvamia tukiwa njiani na kuanza kutushambulia,” alisema ofisa huyo.
Aliongeza kuwa katika kundi hilo la viongozi wa wilaya, walikuwa na askari wawili tu, huku mmoja ndiye aliyekuwa na bunduki, ambapo licha ya kupiga risasi hewani kuwatawanya, wafugaji hao walizidi kuwashambulia.
“Askari yule alipoona maisha yake yako hatarini ndipo alipoanza kuwafyatulia risasi wananchi hao na kumpata mmoja na kufariki huku wengine wote kukimbia,” alieleza
Wakati huo huo, zaidi ya wafugaji 400 wa Kijiji cha Mabwegele Kata ya Kitete, Tarafa ya Magole Wilaya ya Kilosa walikusanyika katika kijiji hicho wakipinga kitendo cha Mkuu wa Mkoa wa Morogoro, Joel Bendera ya kutenguliwa uamuzi wa Mkuu wa Wilaya ya Kilosa kukipandisha hadhi na kuwa kijiji kamili, jambo ambalo lilizua vurugu kubwa katika mji mdogo wa Dumila jana.
Akizungumza na gazeti hili Mwenyekiti wa Kijiji cha Mabwegere wilayani Kilosa, Sharifu Kasenga alisema kuwa wafugaji hao wamekusanyika katika kijiji hicho baada ya kusikia taarifa za uharibifu wa mali za wafugaji katika mji wa Dumila wakati wa vurugu.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Morogoro, Faustine Shilogile alilieleza gazeti hili kuwa hali ya amani imerejea katika mji mdogo wa Dumila pamoja na kitongoji cha Mabwegere.
Imeandikwa na Florence Majani, Dar Mwanja Ibadi, Masasi, Juma Mtanda, Venance George, Morogoro

MMEA UNAOAMINIKA KUONGEZA AMA KUKUZA MAUMBILE YA SEHEMU ZA SIRI WAGUNGULIKA

 
KWA kutumia mabango, lengo likiwa kutangaza kazi zao, waganga wengi wa tiba asilia wamekuwa wakijinadi kuwa wanatoa tiba ya kurefusha maumbile ya siri ya wanaume, kukuza makalio au matiti.
Katika mitaa ya miji na majiji nchini, siyo jambo la ajabu kukutana na mabango hayo, ambayo hata hivyo kushamiri kwake kunaleta picha kwamba ni kutokana na uhitaji mkubwa wa huduma hiyo nchini, huku watoa huduma husika wakinufaika kwa kujikusanyia kiasi kikubwa cha fedha kutoka kwa wahitaji.
Pia dawa zinazodaiwa kukuza makalio maarufu kama ‘mchina’, zimekuwa gumzo baada ya kuingia nchini, huku zikielezwa kukosa ubora na kwamba zina madhara makubwa.
Lakini, sasa unaweza kuachana na dawa hizo za Kichina, baada ya kugundulika mmea wenye uwezo wa kukuza makalio, matiti, pamoja na kurefusha uume.
Taarifa za kiutafiti zinautaja mti huo kwa jina la Mvunge, ukiwa na uwezo wa kukuza makalio, matiti na kurefusha uume.
Kaimu Msajili wa Tiba Asili na Tiba Mbadala nchini, Dk Naomi Mpemba anasema kuwa mmea huo ambao huwa ni mti mkubwa upo na kwamba una uwezo mkubwa wa kukuza maumbile hayo.
Anabainisha kuwa mmea huo ambao hukua na kuwa mti mkubwa huzaa matunda yanayotumika kama dawa na unapatikana wilayani Korogwe Mkoa wa Tanga, Pwani, Mbeya, Morogoro na baadhi ya mikoa nchini.
“Tulifuatilia na kutambua kuwa mti huo upo maeneo hayo na unatumiwa zaidi na waganga, hata picha za mti huo tunazo,” anasema Dk Mpemba na kuongeza:
“Jina jingine unaitwa Miegeya, mara nyingi unastawi katika maeneo yenye ardhi ya unyevunyevu, una tabia ya kustawi kama Mwembe na matunda yake huonekana kufanana na Mbuyu.”
Hata hivyo, anasema kuwa asilimia kubwa ya waganga wa tiba asili na tiba mbadala wanaotumia dawa hiyo ni wale wasiokuwa na usajili kutoka baraza hilo, hivyo kufanya huduma hizo kinyume cha utaratibu.
“Kwa mujibu wa masharti yaliyopo katika agizo la Serikali kwa waganga hao, miiko, maadili na utendaji wa kazi zao umeelekeza kuwepo na usiri na kuaminiwa, kwa hiyo sisi tunaamini wanaojitangaza kutibu mambo hayo ni matapeli,”anasema Dk Mpemba.
Wasiwasi
Huku akionyesha wasiwasi wa kutoa picha za mti huo, Dk Mpemba alisema kwamba endapo utaonekana wazi kupitia vyombo vya habari, jamii inaweza kuathirika kwa sehemu kubwa kuutafuta.
Dk Mpemba alitahadharisha kuwa matumizi ya mmea huo siyo mazuri kwa vijana, badala yake akasisitiza matumizi ya lishe bora kupitia vyakula vinavyojenga mwili.
“Suluhisho ni lishe na siyo kuhangaika na dawa za ajabu, tatizo lenu vijana vyakula ni chipsi, mayai, nguvu zikiwaishia matokeo yake ndiyo mnaanza kutafuta dawa za kurefusha sehemu za siri, haitawasaidia, dawa ni lishe tu,”alisisitiza Dk Mpemba.
Mkuu wa Kitengo cha Utafiti wa Tiba za Asili wa Taasisi ya Utafiti wa Tiba nchini NIMR, Dk Hamis Malebo, alisema Nimr inaufahamu mmea huo, ingawa haijaufanyia utafiti wa kuthibitisha uwezo wake huo.
Alisema mmea huo kisayansi unaitwa Kigelia Africana na unapatikana katika maeneo mengi ya Afrika.
“Masuala ya tiba asilia yanaweza wakati mwingine kuwa na utata na sisi hatuwezi kusema sana kwa sababu hatujafanya utafiti,” alisema Dk Malebo.
Alisema Nimr haiwezi kuzungumza kwa undani kwa sababu bado haijawathibitisha watu waliowahi kupata tiba ya mmea huo, wala haijahakiki chochote kuhusu matunda au mizizi ya mti huo kufanya kazi.
CHAMA
Mkurugenzi wa Kampuni ya Boresa na Mratibu wa Chama cha uratibu wa dawa za tiba asili Tanzania, Boniventura Mwalongo anasema:
“Serikali ifanye majadiliano na kuchunguza, kisha ieleze sasa kama mwanaume kuwa sehemu fupi za siri ni tatizo, au mwanamke kuwa na makalio madogo ni tatizo kwa sababu ya mazingira yalivyo kwa sasa kwenye jamii.”
Mwalongo alikiri kuwepo kwa tatizo hilo na kusema kuwa uchunguzi unahitajika, ili kutofautisha ugonjwa na maumbile ambayo mtu alizaliwa nayo, ili kutoa msaada wa huduma hiyo kama walivyo wagonjwa wengine.
“Kwa sasa kinachofanyika ni utapeli tu, kwa sababu huwezi kujua kama ni ugonjwa au ni maumbile. Kwa nini mtu aongezewe ukubwa wa maumbile yake wakati alizaliwa hivyo?” alisema akihoji na kuongeza:
“Endapo itabainika kweli kuna ugonjwa, watu wanapungua ukubwa wa sehemu zao za siri, basi kunahitajika huduma hiyo.”
Mwalongo alisema kuwa mbali na kuwepo kwa dalili za uhitaji wa huduma hiyo nchini, haoni kama kuna ulazima wa Serikali kushughulikia suala hilo, badala yake akataka iwekeze katika matibabu ya huduma nyingine.
“Kuna magonjwa mengi sana ya zamani na yaliyoendelea kuibuka kwa sasa, kuna magonjwa yanayosababishwa na unywaji na ulaji mbovu, dhambi na ukosefu wa mazoezi, ili kuepusha gharama ya magonjwa haya Serikali inatakiwa kuwekeza elimu kwa jamii,”alisema Mwilongo.
Kauli ya Serikali
Mbali na kukithiri kwa matibabu ya dawa hizo, Serikali imeendelea kutoa onyo kali kwa waganga wote wanaotoa huduma bila kusajiliwa kama ilivyoagizwa.
Matumizi mengine ya Mvunge
Uchunguzi uliofanywa na gazeti hili unaonyesha kuwa mti huo umekuwa ukitumika kwa miaka mingi, ambapo baadhi ya wazazi ama vijana binafsi huamua kwenda kwa wataalamu wa tiba za asili na kupatiwa huduma hiyo baada ya kubainika kuwa maumbile yao kuwa madogo isivyo kawaida.
Mti huo pia unaelezwa kutumika kuponya wazee ambao viungo vyao vimepoteza uhalisia wake pamoja na kutibu ugonjwa wa kuziba njia ya haja ndogo, ukipata umaarufu katika maeneo ya Wilaya za Handeni, Kilindi na Bagamoyo mkoani Pwani,ambapo hupatikana zaidi maeneo ya mabondeni.
Mizizi, matunda, mbegu za matunda, magamba ya mti na majani vyote hutumika kama dawa na chakula.
Matunda yaliyoiva na mabichi ya mti huo ni sumu kwa binadamu, lakini baadhi ya watu hukausha matunda hayo na kuyachanganya katika pombe za kienyeji ili kuongeza ladha.
Karibu kila sehemu ya mti huu hutumika kama dawa ya asili, kwa mfano kulainisha chakula, kutibu kushindwa kupumua, kutibu majeraha na maradhi ya ngozi.
Utafiti wa mti huo katika kutibu bakteria, fungasi na uvimbe unaendelea kufanyika katika nchi za Korea, Japan na India.
Ushuhuda
Mmoja wa watu wanaotoa tiba hiyo ya asili wilayani Handeni Mkoa wa Tanga, akifahamika kwa jina la Dk Ramadhani Chenyewe, anasema kuwa ametibu watu wengi wakiwamo vijana na wazee kutoka ndani na nje ya wilaya hiyo, waliohitaji kuimarishwa nyeti zao.
Chenyewe ambaye pia ni Mwenyekiti wa Chama cha Waganga wa Jadi (MACO) wilayani Handeni, anafafanua kwamba, kwa kutumia dawa hiyo msimu wa mvua nyingi, nyeti hukua kwa haraka katika muda usiozidi mwezi mmoja, kutokana na tunda la mti huo kukua haraka.
“Hilo jambo ni la kweli wengi ninaowatibu wana tatizo uume ni mdogo, na wengine nao ni wazee ambao wanaona mabadiliko katika sehemu hizo kwa kuwa ndogo, tofauti na awali. Basi wakija huwa ninangalia kwanza kama kweli ni ndogo, baada ya kuthibitisha ndipo ninamuongezea,” anasema Dk Chenyewe.
Aliongeza: “Nimewasaidia wengi, tiba yenyewe ni kwamba unakwenda kwenye mti kabla ya kufanya chochote, unaufanyia kitu kama tambiko, baada ya hapo ndipo shughuli ya tiba zinaanza kwa kutumia pia matunda ya mti huo ambayo yanakua kwa urefu.”
Hata hivyo, anaonya kuwa kazi hiyo inahitaji uangalizi mkubwa kwa vile inaweza kuwa kubwa kupita kiasi, hali inayoweza kusababisha madhara kwa mwenza.
Amewataka wanajamii kuacha kwenda kwa waganga kukuza nyeti zao kwa nia ya tamaa ya kutaka kuwakomoa wenzi wao, akisema hilo siyo kusudio la kuanzishwa kwa tiba hiyo ya aina yake.
Mmoja wa watu waliopatiwa tiba hiyo ya kukuza nyeti, ambaye ni mkazi wa mjini Handeni, aliyeomba jina lake lisitajwe, anasema kwamba alikwenda kwa waganga hao kutokana na kuona kiungo chake hakilingani na vya wenzake.
“Mimi wakati tunacheza na wenzangu hasa kwenda kuogelea, nilikuwa nashangaa mbona ya kwangu ni ndogo sana ukilinganisha na wenzangu. Nikamweleza babu yangu, ambaye naye aliniangalia kisha akanishauri twende kwa mganga ambaye anakuza kwa kutumia yale Mavungwe,” anasema kijana huyo mwenye umri wa miaka 27.
Kijana huyo anadai kwamba alitibiwa na kufikia malengo yake kwa muda wa mwezi mmoja, tangu kufanyiwa tiba katika mti huo maarufu sana kwa waganga wa jadi mkoani Tanga.
 

HABARI NA PICHA ZA MATUKIO YANAYOTOKEA MTWARA, SOMA UPATE UNDANI ZAIDI. BOFYA HII LINK

.
POLISI jana wamelazimika kupiga mabomu ya machozi kutwa nzima katika kata ya Chikongola Manispaa
ya Mtwara Mikindani kutawanya wananchi walioizingira nyumba ya diwani wa kata hiyo Mohamedi Chehako kwa madai ya kuwahifadhi wachawi ndani ya nyumba yake, huku mwandishi wa habari mmoja wa Channel 10 akiripotiwa kujeruhiwa.Habari ambazo hazijathibitishwa na kamanda wa polisi mkoani ni kwamba zinadai kuwa majira ya saa 10 kasoro za jioni watu wanaodaiwa kuwa ni wanajeshi wa Jeshi la Wananchi Tanzania (JWTZ) waliingilia kati na
kuanza kutembeza mkong’oto kwa wananchi ili kuzima vuguvugu hizo.
Mwandishi wa hizi habari lipojaribu kuwasiliana na kamanda Nzuki kwa njia ya simu za mkononi hakuweza kupatikana lakini kwenye line nyingine ni kwamba wananchi walitoa tuhuma hizo baada ya kukuta ungo ikiwa na tunguri ndani yake
ambayo inadaiwa kuwa ni ndege ya wachawi uwanjani kwake maeneo ya makaburi Msafa.
Wananchi walijikusanya nyumbani kwa Diwani huyo na kumshinikiza awatoe wachawi nje ili waweze kuwaadhibu amri
iliyopingwa na Diwani huyo, muda ulivyozidi kwenda ndivyo wananchi walivyozidi kuongezeka na hatimaye kulijitokeza kundi la watu walioanza kutia vurugu hali iliyomlazimu Chehako kuomba msaada wa polisi.
Mashuhuda wa tukio walimweleza mwandishi wa habari hizi kuwa polisi walipofika waliwasihi wananchi kutawanyika kwa kuwa ungo na tunguri zake zilikuwa zimeteketezwa kwa moto na diwani huyo mbele ya wananchi hao.
Chenako akihojiwa nyumbani kwake alisema Wananchi waliendelea kupinga na kudai ndani ya nyumba kuna rubani na abiria wa ndege amewahifadhi… polisi wakawachagua wananchi watano na kuingia ndani ya nyumba kuwasaka watu hao lakini hawakuona kitu, walitoka nje na kuwambia wenzao lakini hawakukubali, walianza kurusha mawe kwenye nyumba ndio polisi wakaanza kupambana nao kwa kuwarushia mabomu.
Chehako alibainisha kuwa ni kawada yake kuamka alfajiri kwa ajili ya sala ya
asubuhi, lakini asubuhi ya jana alishindwa kuamka mapema, hata hivyo
hakuweza kuhisi jambo lolote.
Katika mapambano hayo ya wananchi na polisi wananchi kwa kutumia mawe wamemjeruhi Mwandishi wa Habari wa Channel Ten Mtwara John Kasembe kwa jiwe kichwani, pia Ofisa mmoja wa polisi ambae hakutaka kutajwa amethibitisha kutokea kwa tukio hilo na kwamba gari moja ya polisi PT 1421 limevunjwa kioo cha mbele kwa mawe.
Wananchi wamechoma moto mahakama ya Mwanzo na kuvunja vioo vya nyumba za waheshimiwa Hawa Ghasia (Waziri, TAMISEMI) na ya Mohamed Sinani (Mwenyekiti wa CCM Mkoa) zilizopo mtaa wa Sinani.
Wakiwa katika mahakama ya mwanzo Polisi walizingirwa na vijana waliokuwa wamebeba
mawe na kufunga barabara zote za kuingia na kutoka Kituo Kikuu cha Mabasi na eneo la Soko Kuu, licha ya kufyatua hewani mabomu ya machozi. (Taarifa imeandikwa na mtwarayetu.blogspot.com)
Mahakama ya Mwanzo.
Mwandishi aliejeruhiwa.
.
.
Picha zote ni kutoka kwenye camera ya mtwarayetu.blogspot.com

LULU APATA DHAMANA LEO, NA WADHAMIN WATAKIWA KUWEKA DHAMANA YA MILLIONI 20


Lulu akiwa anaingia Mahakamani leo january 28 2013 akiwa na shauku ya kupata dhamana.
Mahakama kuu leo imetangaza dhamana ya mwigizaji Lulu lakini iwapo atatimiza masharti aliyopangiwa ambayo ni pamoja na kuwasilisha hati yake ya kusafiria, kutosafiri nje ya Dar es salaam, kujiwakilisha au kuripoti mahakamani kila siku ya kwanza ya kila mwezi pamoja na wadhamini wake wawili ambao kila mmoja adhamini kwa shilingi milioni 20 za kitanzania.
Upande wa familia ya Lulu umesema masharti yote yaliyotajwa wanaweza kuyatimiza leo leo hivyo wanasubiri tu jibu la msajili ambae ndio anatakiwa kuhakikisha hayo masharti yametimia kisha ruhusa ya kumkabidhi Lulu kwa familia yake itolewe.
Taarifa za ndani ni kwamba uwezekano wa Lulu kuachiwa upo kuanzia january 29 2013 ambayo ni kesho kwa sababu kuna watumishi wawili wa serikali ambao wapo kikazi mkoani Pwani na ndio walitakiwa kutia saini dhamana ya Lulu wakiwa ni sehemu ya masharti.

.

.

.

Hapa ni wakati alipocheka sana pale mwandishi mmoja wa kike ambae pia alikua akimpiga picha alipokua akimlainisha Lulu kwa maneno baada ya mwigizaji huyo kuficha uso wake alipokua akipigwa picha, alisema alikua anaumizwa macho na mwanga wa kamera.

.

.

Mama mzazi wa Lulu ni mwenye nguo nyeupe na nyeusi.

Friday, January 25, 2013

TAARIFAA JUU YA DHAMANA YA MSANII LULU ILIYOKUA ITOKE LEO NI HII HAPA



Elizabeth Michael.
Jana kwenye Exclusive on millardayo.com kulikua na stori kwamba uwezekano wa mwigizaji Lulu kuachiwa kwa dhamana january 25 2013 ulikuepo.
Ni kweli ilikua iwe hivyo lakini kwa taarifa  zilizotolewa kwa Millard Ayo ni kwamba dhamana hiyo imeshindikana kutolewa leo.
Sababu kubwa ni leo kuwa sikukuu hivyo shughuli imesogezwa mbele mpaka jumatatu january 28 2013.
Mwanzoni Lulu ambae anatuhumiwa katika kesi ya mauaji bila kukusudia ilidaiwa alikua anatakiwa apate dhamana ambayo milioni 20 zilihitajika (kwa mujibu wa taarifa za ndani) ila ikashindika sababu jaji alipata udhuru.
Lulu amekua chini ya ulinzi toka kifo cha mwigizaji staa wa movie Tanzania Steven Kanumba April 2012.

Wednesday, January 23, 2013

HUYU NDIE MWANAMKE MWENYE MAPAJA MAKUBWA (HIPS) KULIKO WOTE DUNIANI. SOMA STORY YAKE NA TUPIA MAONI YAKO HAPA





LOS ANGELES, Marekani
WAKATI wanawake wengi duniani wakihangaika kukuza ukubwa wa makalio yao, huku wengine wakitumia njia ya kuvaa taiti zenye hipsi, wanaume wengi huko mjini Los Angeles wamejikuta  wakigeukageuka kumwangalia mwanamke mwenye makalio makubwa kupita kiasi kila apitapo njiani.
Mikel Ruffinelli ni mwanamke ambaye mpaka sasa ‘ameishavunja shingo’ za wanaume wengi. Makalio yake na hispi zake za asili zimemfanya atawazwe kuwa mwanamke mwenye hipsi kubwa kuliko wanawake wote duniani.
Mikel anayeishi nchini Marekani hajatumia dawa za mchina wala dawa zozote kama wafanyavyo akina dada wengine na ndiye aliyetambulishwa kuwa ndiye mwanamke mwenye hipsi kubwa kuliko wanawake duniani. Mpaka sasa mama huyo mwenye familia yake ana  hispi zenye  mita 2.44.
Umbile lake halikuja hivihivi, bali alikuwa ni mtu mwenye umbile la kawaida, licha ya kukiri kuwa ndugu zake wengi wana maumbile makubwa.
Hipsi za mwanamama huyo zimekuwa zikiongezeka siku baada ya siku kadiri alivyokuwa akijifungua watoto wake.
Mikel Ruffinelli, ambaye ni mama wa watoto wanne ana umri wa miaka 39 na ni mkazi wa Los Angeles amejisifia kuwa umbile lake limekuwa likiwachanganya wanaume wengi.
Akiwa na kiuno kidogo kisichoendana na mwili wake cha inchi 40, hispi zake zina mzunguko mkubwa wa inchi 96.
“Nalipenda umbile langu na sina mpango wa kujikondesha kwa diet,” alinena Mikel na kuongeza kuwa wanaume wengi wanapenda wanawake wenye maumbile makubwa siyo wale wembamba wembamba.”
Lakini kauli hiyo, imepingwa vikali na Jennifer Lopez, Kim Kardashian na Beyonce ambao wanasema inategemea na mwanaume husika na namna kile anachokipenda, lakini wakati mwingine hutegemea na mazoea ya mwanamume.
Mikel pamoja na kutamba na maumbile yake hayo ambayo anadai ni urithi toka kwenye familia yake ambapo karibuni ndugu zake wote wa kike nao wana hispi kubwa.
Mikel amelazimika kuishi tofauti ili aweze kuendana na umbile lake, hawezi kuenea kwenye gari ndogo hivyo gari analoliendesha ni kama lori.
Akiwa nyumbani kwake inabidi akae kwenye makochi yaliyotengenezwa kwa chuma badala ya mbao, pia kitanda chake nacho ni futi saba kwa saba.
Mume wa Mikel, Reggie Brooks mwenye umri wa miaka 40 ameelezea kupagawishwa na umbile la mkewe na ameongeza kuwa kila siku humsifia kwa kumwambia jinsi gani alivyo mrembo.
Mikel na mumewe wapo kwenye ndoa kwa miaka 10 sasa na wamefanikiwa kupata watoto watatu ambapo mtoto wa kwanza wa Mikel alizaliwa katika ndoa yake ya kwanza kabla hajaachika na kuolewa na Reggie.
Mikel ameongeza kuwa kwa miaka mitano iliyopita amekuwa akijiingizia kipato chake kwa kupiga picha za mavazi kwa ajili ya Tovuti ya Big Beautiful Women ambapo katika kila wakati anapoitwa kupigwa picha hulipwa Dola 1,000.
Anasema, “Mara nyingi ninapokuwa katika picha za tovuti, ninajitahidi sana kuchagua nguo zitazonifaa. Hivyo wabunifu wananifunza kuuelewa mwili wangu na nguo ipi inaufaa, nami sina tatizo katika suala la uvaaji.”
Mikel Ruffinelli, mwenye uzito wa kilogramu 191 amekuwa na unene uliozidi tofauti na urefu alionao.
“Ninaipenda shepu yangu na sina matatizo ya kiafya hivyo sioni sababu ya kupunguza mwili kwa kujinyima kula na wakati huu nina mpango wa kuongeza mlo ikiwezekana,” anasema Mikel ambaye hula kuku mzima na vyakula vingine vya wanga na protini kwa siku.
Mazoezi ya Mikel hutegemea na siku husika, mara nyingi anasema hufanya matembezi ya jioni akiwa na mume wake na wakati mwingine huamua kutembea sehemu moja hadi nyingine kuzunguka nyumba yake.
Mume wake ambaye ni mtaalamu wa masuala ya kompyuta anasema anavutiwa zaidi na mkewe na hapendi kabisa apungue mwili na anadhani ni mwili mzuri tu kwa kuwa hajatumia madawa kuukuza.
Alipokuwa na umri wa miaka 22, Mikel alipata mtoto wake wa kwanza Andrew ambaye hivi sasa ana miaka 19, kutoka katika uhusiano uliopita na hapo ndipo alipoanza kuongezeka uzito.
Alianza kwa kuongezeka kilo 82.5 na baadaye alifikia kilo 108. Baadaye alikutana na Reggie na baada ya miongo mitatu sasa wana watoto watatu. Destynee, 13, Autumn, nane na Justyce, saba. Na hivi sasa hipsi zake zimetanuka mpaka kufikia uzito wa kilogramu 191.
“Nilikuwa nikiongezeka nikiwa na ujauzito.  Sikujua ni kwa nini uzito uliongezeka sana na hipsi kuwa kubwa, niliendelea kula zaidi, lakini nilivyojifungua sikuweza kurudia mwili wangu wa awali, hivyo ndivyo ilivyokuwa.”
Mikel, ambaye alisomea Shahada ya Saikolojia, ni mwenye afya na hamu kubwa ya kula na anayeweza kumaliza chakula kingi kwa siku.
“Ni maajabu kuona mwanamke anakula kalori 3000 kwa siku lakini kwangu mimi ni jambo la kawaida.
“Ninapata kifungua kinywa cha mayai mawili, soseji na viazi kadhaa. Mchana chakula changu kikubwa ni samaki wa kukaanga na chakula cha wanga kingi tu, lakini chakula cha jioni huwa ninahitaji zaidi mlo mzito.
“Ninapenda kutengeneza kuku wa kuoka wawili wakubwa na wali. Nina fungu kubwa, lakini ninapenda chakula kizuri, ninaandaa pia vitafunwa kama karanga, klipsi na vingine vinavyoweza kuliwa usiku.”

sikiliza ngoma zinazo kamata kwa sasa

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...