Tuesday, January 8, 2013

Mrithi wa mali achinjwa mithiri ya kuku, Kilimanjaro


WATU wasiojulikana wamemuua kikatili kijana mmoja mwenye mtindio wa ubongo kwa kumchinja na kutenganisha kichwa na kiwiliwili na pia kukata mguu mmoja na kuutenganisha na kiwiliwili.
Hata hivyo kichwa pamoja na mguu huo ulikutwa eneo la tukio sambamba na kiwiliwili hicho,  huku wananchi wengi wakiamini kuwa kilichomuua ni kitendo cha baba yake kufa na kuacha mali kadhaa ambazo mrithi mkubwa ni kijana huyo.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kilimanjaro, Robert Boaz aliwaambia waandishi wa habari kuwa mauaji hayo yaligunduliwa Ijumaa iliyopita baada ya kuokotwa kwa mwili wa kijana huyo chini ya daraja.
Mwili wa kijana huyo, Emannuel Vicent Chuwa (25) ambao ulishaanza kuharibika ulikutwa chini ya daraja linalounganisha Vijiji vya Kibosho Singa na Kibosho Sungu vilivyopo Wilaya ya Moshi Vijijini.
“Kwa mujibu wa maelezo ya ndugu wa marehemu wanasema kijana huyo aliyekuwa akilelewa na baba yake mdogo alikuwa haonekani kwa siku tisa mfululizo hadi mwili wake ulipopatikana,” alisema Boaz.
Baba mzazi wa kijana huyo ni marehemu na alipofariki alimwachia urithi wa mali nyingi kijana huyo.
Kamanda Boaz alisema polisi wameanzisha uchunguzi kuhusiana na tukio hilo la kinyama na inawashikilia baba mdogo na mama mdogo ambao waliachiwa wosia wa kumlea marehemu huyo.

No comments:

Post a Comment

sikiliza ngoma zinazo kamata kwa sasa

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...