Friday, February 1, 2013

LAIBONI; MIAKA 103, WAKE 40, WATOTO 113, WAJUKUU LUKUKI!



ASILIMIA 60 ya watu duniani huamini kuwa hadhi ya mtu kwenye jamii ni kuwa na fedha, magari au nyumba.
Hata hivyo , kwa Mzee Meshiko Mapi, Mmasai mwenye umri wa miaka 103, kwake maisha mazuri na yenye hadhi ni wake zake wengi, watoto, wajukuu na ng’ombe wengi wa kutosha.
Unapoingia katika eneo lake unamkuta mzee huyu akiwa  katika himaya yake ya kifahari, katika Kijiji cha Esilalee, Wilaya ya Monduli Mkoani Arusha. Himaya hiyo ipo katikati ya eneo la Miji midogo ya Makuyuni na Mto wa Mbu.                  
Magari yote ya abiria yanayopita  kijijini Esilalee kwenda maeneo mengine, yanakifahamu kituo  maarufu  cha kwa ‘Laiboni.’
Laiboni, ni jina  maarufu la Mzee Mapi na  yeye ndiye mmiliki wa kijiji hicho kwani wakazi wote wa kijiji hicho  ama ni watoto au wajuku zake.
Si hivyo tu, bali Shule ya Msingi Laiboni iliyopo katika kijiji hicho nayo ni ya kwake na  baadhi ya wanafunzi  wa shule hiyo ni watoto na hata wajukuu zake.  Kijiji hiki kimepambwa kwa mandhari yenye nyumba ndogondogo za msonge. Ni nyumba tatu tu kati ya hizo, ndizo zilizojengwa kwa matofali na kuezekwa kwa bati.
Nyumba ya  Laiboni, ambayo ni ya kisasa, ipo katikati ya kijiji, zizi la mifugo limejengwa mbali kidogo, kiasi cha hatua 100 kutoka zilipo nyumba nyingine.
Ingawa ni siku ya Jumapili, lakini kijiji hicho kimetawaliwa na ukimya mwingi. Shinini Mapiko Mapi, mtoto wa 82 wa Laiboni, ambaye ndiye mkalimani wangu anasema wanafamilia wengi wamekwenda katika shughuli zao, zikiwamo za kuchunga mifugo na nyinginezo. Karibu wakazi wote katika kijiji hiki hawafahamu Kiswahili, baadhi  wanayafahamu maneno machache na kuelewa lugha hiyo kwa kiasi kidogo.
Hata hivyo, Shinini peke yake ndiye anayeielewa  lugha ya Kiswahili ukilinganisha na wengine na yeye anakuwa msaada mkubwa kwangu, kama mfasiri.
Nzi, wadudu ambao hupenda mazingira yenye majimaji, maziwa au wanyama ndiyo wanaokukaribisha mahali pale, bila shaka wanasababishwa na wingi wa ng’ombe zaidi ya 2500  mali ya  Laiboni, ni kero kwa wageni na pengine hata kwa wakazi hao.
Unakutana na Laiboni, ameketi na watoto wake wa kiume 11, ambao ni sawa na timu ya mpira wa miguu.
Wengine wanacheza bao, baadhi wamejilaza huku wakiendelea kuwafukuza nzi waliokithiri.
Laiboni, mwenyewe ameketi kwenye kiti cha ngozi naye akifukuzana na nzi kwa kutumia usinga wa mkia wa ng’ombe.
Mwenyeji wangu, Shinini ananiambia nimsalimie kwa kumpa kichwa. Ninafanya hivyo naye anaweka mkono kichwani mwangu. Hizo ni salamu za Kimasai.
Laiboni anasema  alizaliwa mwaka 1910, katika Kijiji cha Olaleni, wilayani Ngorongoro.
Alikulia katika mazingira yaliyoheshimu mila na tamaduni. Alifundishwa kuthamini mifugo, alifundwa kuwa shupavu na jasiri kwa kuwa yeye ni mwanamume.
“Mwanamume usipokuwa jasiri, unadharaulika, unailetea familia yako aibu,” anasema akiendelea kuwafukuza inzi.
Laiboni anasema alioa mke wa kwanza akiwa na miaka 21, na anamkumbuka vyema mke huyo ambaye aliitwa Naitiame Ngishwa. Kwa bahati mbaya,  Naitiame hivi sasa ni marehemu.
“Hilo ndilo lilikuwa chaguo langu la kwanza… Naitiame Ngishwa,” anasema Laiboni.
Anasema kwa kuwa alibahatika kuwa na ng’ombe kiasi alioachiwa na baba yake mzazi mzee Mapi, hakuona sababu ya kuwa na mke mmoja- aliongeza wa pili.
“Fahari ya Maasai ni kuwa na wake wengi, kama una ng’ombe, unaoa mpaka ushindwe mwenyewe,” anasema mzee huyo ambaye pamoja na umri wake, meno yake mengi bado ni imara.
Shinini anasema mila za Maasai zinamtaka mwanamume mwenye wake wawili au zaidi kuwa na nyumba yake mwenyewe, kisha wake zake nao kuwa na nyumba zao.
“Unajua wanawake wanajenga ‘manyata’ zao wenyewe, na mzee wa boma anakuwa na nyumba yake,” anasema. Laiboni anasema   kadri siku zilivyokuwa zikikimbia Mungu alimbariki  na mifugo yake iliendelea kuongezeka. Kadri mifugo ilivyokuwa ikiongezeka ndivyo naye alipata ari ya kuoa zaidi. “Fahari yetu ni wake, mifugo na watoto, hakuna kitu kingine,” anasema.
Anasema aliendelea kuoa hadi sasa ana wake 40, ingawa baadhi wamefariki na wengine wamezeeka. Anajaribu kuwataja baadhi ya wake zake ambao ni pamoja na Naitiame, Nakaaye, Meeki, Ndemero, Supana, Mosipa, Naishooki, Meshi, Siyama na Mama Saunya.
Mke mdogo wa Laiboni ni  Meshi, ambaye kwa sasa ana miaka 42.
Laiboni anasema  kutokana na yeye kuwa na wake wengi, alibahatika kupata watoto wengi pia. Watoto wa Laiboni kwa  hivi sasa wanakadiriwa kuwa ni zaidi ya 103, hao ni baada ya wengine kufariki dunia.
“Kila mwanamke lazima azae watoto wengi, kila mwanamke ili aheshimike ni lazima awe na watoto saba na zaidi,” anasema.  Hata hivyo, anasema mke wake wa kwanza, Naitiame, hakuweza kuzaa watoto wengi, bali watatu tu.
Mtoto wa kwanza wa Laiboni, ambaye ni mwanamke, hivi sasa ana umri wa miaka 72 na anaishi   Wilaya ya Karatu.
Ratiba yake  Laiboni hula katika kila nyumba  ya mke mmoja kila siku. Asubuhi hunywa chai katika nyumba moja, mchana nyingine na jioni hula na kulala katika boma nyingine.
“Ninahakikisha nawatembelea wote, siwezi kusahau au kupitiwa,” anasema huku akicheka. Anasema kila mwanamke ana ng’ombe wake, ambao hutakiwa kuwachunga, hata hivyo dhamana ya kuuza ipo kwa watoto wake wa kiume . Shinini anasema:”Kila inapofika siku ya mnada, ng’ombe au mbuzi hupelekwa kuuzwa, hata hivyo bado idadi yao inazidi kuongezeka kwani wanazaliana,”
Rafiki wa Lowassa na Sokoine
Laiboni, pengine kutokana na utajiri wake wa mifugo, alipata kujuana na watu mashuhuri, akiwemo  aliyekuwa Waziri Mkuu katika uongozi wa Mwalimu Julius Nyerere, Edward Sokoine (marehemu). Si hivyo tu, bali  Laiboni anasema yeye ni rafiki wa karibu wa Waziri Mkuu aliyejiuzulu, Edward Lowassa. “Lowassa ni rafiki yangu mkubwa, aliwahi kunichukua tukaenda wote nchini Uganda kwa Rais Yoweri Museveni,” anasema
Shule ya Msingi Laiboni
Kwa kutumia utajiri wake wa ng’ombe, Laiboni alichukua uamuzi wa kujenga shule ya msingi kwa ajili ya watoto na wajukuu zake.
Kwa bahati nzuri, hakufanya kazi hiyo peke yake, bali alipata msaada toka kwa Shirika la Kusaidia Watu la Marekani,USAID. Laiboni kwa kuwa hakuwahi kusoma, hafahamu vyema kuhusu USAID, lakini anawashukuru kwa msaada wao, uliowezesha kizazi chake kupata elimu. “Niliuza ng’ombe, tukapata fedha za kuanzisha shule ingawa nilisaidia na USAID, nia ni kutaka watoto wangu wasome, hapa hakuna shule nyingine zaidi ya hii,” anasema
Shule ya Msingi Laiboni ina vyumba saba vya madarasa. Inao wanafunzi 130, kati ya hao 25 ni watoto wake 17, wajukuu na wanafunzi  wengine wanatoka vijiji vya jirani.
Shinini anasema  walimu wa shule hiyo wanalipwa na Laiboni mwenyewe kwa kusaidiwa na USAID.
“Walimu wengine wanatoka serikalini na wengine wanalipwa na mzee mwenyewe,” anasema kijana huyo. Laiboni anasema:  “namshukuru Mungu kwani kila kitu nilichotamani kukipata duniani nimekipata, haja zangu kuu zilikuwa ni ng’ombe, wake na watoto… na vyote nimepata.”
Picha hapana!
Lakini, Laiboni anakataa kupiga picha na wake zake akidai kuwa mila za Wamasai haziruhusu wanawake kuchangamana na wanaume.
Mzee huyo akaruhusu kupigwa picha na watoto wake saba, wakubwa wa kiume ambao anaeleza kuwa ndio wasaidizi wake.

No comments:

Post a Comment

sikiliza ngoma zinazo kamata kwa sasa

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...