
Mtoto wa kwanza wa Hayati Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere 
aitwaye Madaraka, amesema viongozi wa sasa wameshindwa kufuata nyayo za 
kiongozi huyo kutokana na sababu ambazo amesema “haziko wazi”.
 
Katika mahojiano yake na gazeti hili, Madaraka 
anasema: “Mazingira ya sasa hayaruhusu malengo ya uadilifu kuenziwa kwa 
sababu nafasi za umma zinakubalika sasa kuwa ni maeneo ya kujinufaisha 
mimi kwanza, halafu Tanzania Mungu akipenda”.
Yafuatayo ni mahojiano kamili na Madaraka.
Mwananchi: Ni miaka 14 sasa tangu kufariki kwa 
Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere, unaizungumziaje miaka hiyo 
kimaisha katika familia, bila kuwapo kwa Mwalimu?
Madaraka: Binadamu tumeumbwa na uwezo wa 
kukabiliana na kuondokewa ndugu na jamaa zetu wa karibu. Majonzi 
yalikuwa makubwa baada ya kufariki Mwalimu, lakini tunatambua kuwa kuna 
umuhimu wa kuomboleza na baadaye kuendelea kukabiliana na changamoto za 
kila siku za maisha. Na yeye angetarajia hivyo.
Mwananchi: Mwalimu Nyerere alikuwa kiongozi wa 
nchi, ni zipi fikra au mtazamo wako jinsi viongozi wetu wa sasa 
wanavyomuezi kwa kuwa wafuasi wa nyayo zake?
Madaraka: Hebu tuseme tu bila unafiki kuwa katika 
masuala mengi ya uongozi, hasa ya uadilifu, suala la kumuenzi Mwalimu 
Nyerere ni lengo ambalo viongozi wengi wa sasa wanaweza kuwa wanalo, 
lakini kutokana na sababu ambazo haziko wazi basi hilo lengo siku zote 
halikamatiki, liko hatua kumi mbele yao. Na kila wakielekea kama 
kulifikia na kulitimiza basi wanateleza na kuanguka na lengo hilo 
linawaacha hatua nyingine 20 mbele.
Mazingira ya sasa hayaruhusu malengo ya uadilifu 
kuenziwa kwa sababu nafasi za umma zinakubalika sasa kuwa ni maeneo ya 
kujinufaisha mimi kwanza, halafu Tanzania Mungu akipenda.
Mwananchi: Miongoni mwa mambo ambayo Mwalimu 
Nyerere aliyaenzi na kuyasimamia enzi za uhai wake, ni Muungano. Kwa 
maoni yako unadhani hili linaenziwa vipi? (rejea mvutano wa sasa wa 
Serikali mbili, tatu nk, unatokana na mchakato wa Katiba Mpya).
Mwananchi: Nitumie msemo wa kisiasa kuwa sasa hivi
 suala la kutengua Muungano linazungumzika. Wakati waasisi wenyewe wapo 
hai wale waliofikiria kutengua Muungano walipata kigugumizi au 
walishindwa kuwa wazi na fikra zao. Sasa hivi inaelekea kuna baadhi ya 
makundi ya viongozi pande zote mbili za Muungano hawataki Muungano, 
lakini wanashindwa kuwa wazi kutetea msimamo wao huo. Ni sauti chache 
sana utazisikia zikisimama bila kutetereka kutetea kuwepo kwa Muungano.
Ni dhahiri kuwa sauti za kutaka Zanzibar iachane 
na Muungano zimekuwa na nguvu zaidi kuliko zile ambazo zinatetea 
Muungano. Naamini kuwa viongozi wanaozungumzia Muungano wa mkataba 
hawajapata ujasiri wa kisiasa wa kusema kuwa hawataki kabisa Muungano.
Naweza kuwa siko sahihi, lakini naamini kuwa 
yeyote anayejaribu kutetea umoja mkubwa zaidi kati ya Bara na Visiwani 
na siyo mfano tu wa umoja anapingana na mtazamo uliojengwa juu ya fikra 
kuwa maendeleo ya Zanzibar yanakwamishwa na kuwepo ndani ya Muungano.
Kwa sababu ni baadhi ya wanasiasa ndiyo wanajenga fikra hizi 
tunaweza kusema kuwa ni siasa ndiyo inasukuma ukweli badala ya ukweli 
kusukuma siasa. Kwa maoni yangu, ukweli wa kisiasa unajengwa juu ya 
kushinda uchaguzi ujao.
 
Hilo ndilo jambo la msingi. Kusimamia ukweli 
tofauti na hapo kunaweza kusababisha kushindwa uchaguzi. Ukweli 
ninaoamini mimi ni kuwa siku zote umoja huleta nguvu, utengano udhaifu. 
Hii ni kweli katika suala la uchumi na hata kisiasa.
Lakini iwapo hilo ndilo wananchi wanataka, huwezi 
kulikwepa. Matokeo yake ni Serikali tatu. Umoja wa kweli ungekuwa 
Serikali moja na sauti za ‘mimi’ na ‘wewe’ (Zanzibar na Bara) zingepotea
 na kuchukuliwa na suala la ‘sisi’ (Watanzania). Lakini suala la 
Serikali moja lilionekana haliwezekani, mwaka 1964 na la Serikali mbili 
likaonekana mwafaka. Kwenda kwenye Serikali tatu ni kama kupiga hatua 
moja nyuma katika kuulinda Muungano.
Mimi nalaumu uwezekano wa kupatikana kwa 
rasilimali ya mafuta kama kichocheo kikubwa cha kuyumbisha Muungano. 
Siku zote pesa na utajiri ndiyo hugombanisha ndugu. Ndugu wenye utajiri 
wana fursa nyingi zaidi za kutoelewana kuliko ndugu wasio na utajiri.
Ukweli ni kuwa kama huna mali hutakuwa na ugomvi 
kuhusu mali na ndugu yako. Mara tulipopata harufu ya mafuta chini ya 
Bahari ya Hindi basi masuala ya kuukosoa Muungano yakapamba moto.
Mwananchi: Nje ya Serikali ambako Mwalimu Nyerere 
alikuwa kiongozi, kuna familia ambako alikuwa baba. Ndani ya familia je,
 mnamuenzi vipi Baba wa Taifa?
Madaraka: Ukiwa ndani familia huna uchaguzi juu ya
 kama unataka kumuenzi Mwalimu au la. Watu watakupachika matarajio yao 
na kiwango cha ulinganishi kimeshawekwa na Mwalimu Nyerere.
Kwa hiyo mwanafamilia anapokuwa na mwenendo ambao 
haufanani na hicho kiwango kinachotarajiwa, basi wengi wanashangaa. 
Mfano, mimi nikivuta bangi nitaandikwa kwenye gazeti, lakini kitendo 
hicho kikifanywa na Mtanzania ambaye baba yake hana wadhifa mkubwa wa 
uongozi hiyo haiwezi kuwa habari.
Labda wengine watasikitishwa na suala hilo. 
Watakaofurahi ni wale ambao wanakubali kuwa uadilifu katika uongozi na 
utumishi wa umma ni suala lisilowezekana.
Baadhi ya wanafamilia tunasimamia kutangaza Kijiji
 cha Butiama kama eneo la kihistoria na la kiutamaduni. Wageni wengi 
bado wanafika kutembelea Butiama mahususi kwa sababu ndipo alipozaliwa 
na kuzikwa Mwalimu Nyerere.
Mwananchi: Ni tabia ya viongozi wengi wa Afrika 
kujilimbikizia mali wanapokuwa madarakani. Ukiwa kiongozi wa familia ya 
Mwalimu Nyerere, unaweza kueleza tofauti yao na Baba wa Taifa? Je, yeye 
aliwaachia mali kiasi gani (kwa maana ya fedha, nyumba na mashamba)?
Madaraka: Awali, mimi siyo kiongozi wa familia ya Mwalimu Nyerere. Hatuna nafasi hiyo ndani ya familia.
Mimi naamini kuwa mtu ambaye hana tamaa ya kujilimbikizia mali 
huzaliwa hivyo. Huwezi kupenda kujilimbikizia mali na utajiri (kwa njia 
halali au vinginevyo) halafu ukakaa madarakani kwa miaka 23 bila tabia 
yako hiyo kujitokeza katika matendo yako au ya wale waliokuzunguka. 
Ukweli utabainika tu.
Sasa inawezekana kuwa kiongozi akashika wadhifa 
akiwa mwadilifu halafu akiwa madarakani akapata vishawishi vya 
kujilimbikizia mali.
Hapa ndiyo natoa hoja kuwa kama wewe ulizaliwa 
kuwa mtu usiyesumbuliwa na kukosa mabilioni ya shilingi kwenye akaunti 
yako basi hivyo vishawishi havitakusumbua. Lakini tofauti ya hivyo 
utashawishika kujitajirisha mwenyewe na kusahau wajibu kwa umma.
Sisi hatukuachiwa mali yoyote ambayo ilitokana na 
kipato chake. Kuna nyumba ile ya Msasani ambayo aliijenga kwa mkopo 
ambao hakuweza kuulipa wakati anastaafu na aliamua kuikabidhi Serikali, 
lakini Serikali ya Rais Ali Hassan Mwinyi ilipitisha uamuzi wa kulipa au
 kufuta deni na akakabidhiwa nyumba. Kuna nyumba ndogo ambayo alijenga 
akiwa Rais, iko Butiama.
Vilevile, baada ya vita vya Kagera alijengewa 
nyumba na Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) ambayo baadaye Serikali 
ilichukua jukumu la kuikamilisha. Awali, ni wanajeshi wenyewe walikuwa 
wanakatwa mishahara yao kuchangia ujenzi wa nyumba hiyo.
Nyumba nyingine ipo Butiama na alijengewa na CCM 
baada ya viongozi wenzake kuamua kuwa nyumba yake aliyojenga Butiama ni 
ndogo sana na haistahili kutumiwa na Rais wa nchi.
Alipewa eneo la shamba na Kijiji cha Buturu, 
jirani na Kijiji cha Butiama, ingawa kumekuwa na mbinu za kutaka kupora 
hilo shamba zinazoongozwa na baadhi ya viongozi wa zamani wa kijiji 
hicho.
Mwananchi: Novemba 2004, familia ya Baba wa Taifa 
ililalamikia Sheria ya Kuwaenzi Waasisi wa Taifa iliyopitishwa na Bunge,
 kwa hofu kwamba ingepoteza uhalali wa kumilikia baadhi ya mali za 
Mwalimu Nyerere. Ni kipi kinajitokeza kama changamoto tangu kupitishwa 
kwa sheria hiyo?
Madaraka: Jibu hili litakuwa refu kidogo kwa kuwa 
lina masuala mengi ndani yake. Mimi nilikuwa mmojawapo wa wajumbe wa 
kamati ndogo ya Serikali iliyoshiriki kwenye kazi ya kuchangia vipengele
 vya muswada wa ile sheria.
Nilikuwa ninaiwakilisha familia pamoja na dada 
yangu Rosemary. Kuna baadhi ya vipengele ambavyo tulipendekeza kama 
familia wakati wa kuandaa muswada na waziri mhusika alienda bungeni 
kutoa tamko tukiamini kuwa mapendekezo yetu yangekuwa sehemu ya sheria, 
lakini waziri alipofika huko hakuchukua mapendekezo yote kutoka upande 
wa familia.
Changamoto siyo nyingi, lakini kuna jambo la 
msingi ambalo nafikiri linahitaji kutolewa uamuzi haraka. Sheria inaweka
 wazi kuwa kazi ya kuwaenzi waasisi wa Tanzania ni jukumu la pamoja na 
kuwa yeyote anayemiliki kumbukumbu za Mwalimu Nyerere na za Sheikh Abedi
 Amani Karume ataendelea kumiliki hizo kumbukumbu, lakini atatarajiwa 
kushiriki kwenye kizitunza kwa mujibu wa sheria hii na sheria nyingine 
zilizopo.