Friday, December 21, 2012

DK SLAA ASEMA TUNASUBILI TAARIFA YA ARFI


KATIBU mkuu wa Chadema, Dk Willbroad Slaa amesema chama hicho kinasubiri kupokea taarifa ya mgogoro unaofukuta ndani ya chama hicho mkoani Katavi na kusababisha Makamu Mwenyekiti wake Taifa , Said Arfi, kutupa kadi yake ya uanachama.

Ameeleza kuwa Katiba ya chama hicho inaeleza wazi kwamba unapoibuka mgogoro, unatakiwa kuripotiwa katika ofisi ya Katibu Mkuu Taifa ndani ya siku 14.

Tukio la Arfi kutupa kadi ya Chadema lilikuwa la pili ndani ya wiki moja, kwani juma lililopita uliibuka mgogoro mwingine wilayani Karatu ambako pamoja na mambo mengine uliishia kwa Kamati Kuu kuusimamisha uongozi wote wa chama hicho wilaya.

Arfi ambaye ni Mbunge wa Mpanda Mjini, alitishia kujitoa Chadema juzi, katika kikao cha Kamati ya Ushauri ya chama hicho Mikoa ya Katavi na Rukwa kilichoketi Namanyere, Nkasi na kufikia uamuzi wa kumsimamisha Mwenyekiti wa Baraza la Vijana Mkoa wa Rukwa, Laurent Mangweshi.

Katika kikao hicho, Arfi anadaiwa kuichukua kadi yake ya Chadema na kumtupia Mwenyekiti wa Chadema Mkoa wa Rukwa, John Mallack akitangaza kuachia nyadhifa zote alizonazo, kisha kuondoka ukumbini, kabla ya kufuatwa na wazee wa chama hicho na kumsihi aichukue kadi yake hiyo.

Hata hivyo, Mangweshi jana aliliambia Mwananchi kwamba hajapewa barua hiyo mpaka sasa na kwamba yeye bado ni Mwenyekiti wa Bavicha mkoa wa Rukwa, kauli ambayo ilipingwa na Katibu wa chama hicho mkoani Rukwa na Katavi, Ozem Chapita aliyesema kuwa ipo tayari na wameisafirisha kwa basi jana mchana ili imfikie.

Akizungumzia tukio hilo jana Dk Slaa alisema  taarifa hizo amezisikia ila hawezi kutoa maamuzi kwa kuwa Chadema kinafuata taratibu za vikao pamoja na Katiba yake.

“Utaratibu wa chama ni kwamba malalamiko yeyote ni lazima yawasilishwe katika ofisi ya Katibu Mkuu ndani ya siku 14” alisema Dk Slaa na kuongeza;

“Mimi kama Katibu Mkuu ni lazima nifuate taratibu za chama na sio kufanya vinginevyo.”

Alisema kuwa taarifa hizo amezisikia kupitia vyombo vya habari na kwamba anachokisubiri ni taarifa rasmi ya maandishi ili kama chama kiweze kukaa vikao na kujadili mgogoro huo.

Alipoulizwa kuna taarifa kwamba baadhi ya makada wa chama hicho wanatumiwa kukivuruga, Dk Slaa alisema kuwa inawezekana hilo likawa na ukweli lakini kama kawaida ya chama hicho, hakitoi maamuzi bila ya kukaa vikao.

“Hizo ni taarifa ambazo zipo na zinaandikwa kila siku katika vyombo vya habari, zikija rasmi katika ofisi ya chama zitajadiliwa” alisema Dk Slaa.

Arfi alifikia hatua hiyo baada ya kutokea sintofahamu kati ya wajumbe wa kikao hicho katika uamuzi huo uliofikiwa kwa kupiga kura za ndiyo na hapana.


Vyanzo vya habari kutoka ndani ya kikao hicho vilifafanua kuwa Arfi alikerwa na kauli iliyotolewa na Mangweshi kuwa katika Uchaguzi Mkuu uliopita, alipokea rushwa kutoka kwa Waziri Mkuu, Mizengo Pinda.

Vyanzo hivyo vya habari vimeeleza kuwa kutokana na hali hiyo, Arfi alipandwa na hasira na kuamua kumrushia kadi Mallack kisha kutoka nje ya ukumbi.

“Hatua hiyo ilifanya wajumbe wa kikao hicho nao kutoka nje ya ukumbi na kuanza kumbembeleza ili asichukue uamuzi huo na kisha wakamwekea kadi yake ya uanachama katika mfuko wake wa shati,” alisema mmoja wa makada hao.

Arfi mwenyewe hakupatikana juzi kuzungumzia tukio hilo na hata jana alipotafutwa simu zake zote zilikuwa zimezimwa.

Mangweshi aeleza ya moyoni

Akizungumzia kitendo cha kuvuliwa madaraka
Mangweshi alisema mara baada ya kukabidhiwa barua yake atakata rufaa kwa maelezo kuwa haki haikutendeka katika kikao hicho.

Alisema mpaka sasa taarifa za kuwa amevuliwa uongozi anazisikia katika vyombo vya habari, huku akisisitiza kuwa yeye bado ni Mwenyekiti wa Bavicha wa mikoa  ya Rukwa na Katavi.

Alipohojiwa juu ya kuonywa mara kadhaa katika vikao kutokana na utovu wake wa nidhamu alisema, “Katika maisha yangu sijawahi kuonywa na hata Chadema sikuwahi kuonywa tangu nilipojiunga mwaka 2001, hakuna kikao cha baraza la uongozi kilichokaa kunijadili.”

Alifafanua kwamba hata Baraza la Usuluhishi halina mamlaka ya kumvua mtu madaraka na kuongeza kuwa  kikao kilichofanyika  Namanyere kilikuwa ni cha Baraza la Usuruhishi na si cha Baraza la Uongozi ambalo alidai kuwa ndio lenye mamlaka.

Alisema ameshangazwa na kitendo cha viongozi  wa Chadema mkoani Katavi kukimbilia katika vyombo vya habari kutoa tamko la kumfukuza kabla ya kukamilisha taratibu za kichama.

“Mimi ndio nilitakiwa kukimbilia katika vyombo vya habari kudai haki yangu kama wangenikabidhi barua yangu, kinyume chake wao ndio wamekimbilia huko tena bila kufuata taratibu” alisema na kuongeza;

“Kama hawatanitendea haki sitahama Chadema, nitafia hapa hapa kwa sababu chama hiki lengo lake ni kulikomboa taifa kutoka mikononi mwa CCM.”

Katibu wa chama hicho mkoani Rukwa na Katavi, Ozem Chapita alikiri kuchelewa kwa barua ya kumvua madaraka  Mangweshi  na kusema kuwa tatizo ni kwamba  mwenyekiti huyo anaishi mkoani Katavi  huyu yeye ambaye ni mtendaji mkuu wa chama hicho akiwa anaishi mkoani Rukwa.

Alisema barua hiyo ipo tayari na wameisafirisha kwa basi ili iweze kumfika Mangweshi.



Tanga kwazidi kufukuta

Katibu wa Bavicha mkoani Tanga, Deogratius Kisandu ameitaka Tume ya Taifa ya Uchaguzi (Nec) kubatilisha Uchaguzi Mkuu wa Rais mwaka 2010  kwa kuwa ulikuwa na wagombea wawili kutoka Chama cha Mapinduzi (CCM).

Alisema kitendo hicho kinatakiw akufanywa haraka baada ya Dk Slaa ambaye aligombea urais mwaka 2010 kwa tiketi ya Chadema kukiri  kwama mpaka sasa bado anayo kadi ya CCM.

“Katika hili ni  ni wazi kuwa uchaguzi mkuu wa mwaka 2010 ulikuwa batili na kulikuwa na wagombea wawili kutoka chama kimoja” alisema Kisandu.

Kisandu aliyasema hayo jana wakati akijibu tuhuma alizotupiwa na Mwenyekiti wa Chadema Mkoa wa Tanga, Said Mbweto  kwamba amekurupa kutoka tamko la kumtaka Dk Slaa ajiuzulu.

“Mara baada ya Dk Slaa kukiri kuwa na kadi ya CCM , Nec inastahili kubatilisha uchaguzi mkuu wa mwaka 2010 na kuitisha upya uchaguzi wa Rais ili wajitokeze wagombea wapya wa nafasi hiyo” alisema Kisandu.

Alisema kwa maana hiyo ni kwamba hata Rais Kikwete kwa sasa hastahili kuwa katika nafasi hiyo kwa sababu kauli ya DK Slaa imebatilisha nafasi yake.

Alisema hakukurupuka kutoa kauli hiyo na kwamba yalikuwa mawazo yake binafsi na kusisitiza kuwa msmimamo wake uko palepale.

Karatu wapitisha bajeti

wilayani Karatu Kamati ya Ushauri ya wilaya ya hiyo (DCC), juzi imepitisha mapendekezo ya makadirio ya mapato na matumizi ya  mwaka 2013/14 ya Halmashauri ya wilaya hiyo, ambapo kiasi cha Sh 20.6 bilioni kinatarajiwa kukusanywa.

Mkurugenzi wa halmashauri hiyo, Clementi Berege akiwasilisha taarifa ya mapendekezo hayo,katika kikao hicho, kilichoongozwa na Mkuu wa wilaya hiyo, Felix Ntebenda, alisema bajeti hiyo ya 20.6 bilioni ni ongezeko la  sh 51.7 milioni ya bajeti iliyopita ya mwaka 2012/13.

Alisema mapato ya ndani ya halmashauri hiyo yanatarajiwa kufikia 1.9 bilioni,Ruzuku ya matumizi ya kawaida 17.3 bilioni na ruzuku ya miradi ya maendeleo 2.1 bilioni.

Hata hivyo, alisema bajeti hiyo, inaweza kubadilika kutokana na maoni na vyombo vingine vya maamuzi, ikiwepo baraza la madiwani na vyombo vingine kabla ya kufikishwa kwenye bajeti kuu.

Akichangia taarifa hiyo, Mkuu wa wilaya hiyo, Ntibenda aliwataka wadau wa maendeleo katika wilaya hiyo, kuendelea kushirikiana na serikali katika kuifanikisha bajeti hiyo.

Hata hivyo, Ntibenda aliwataka watendaji na halmashauri na wanasiasa kushirikiana kwa pamoja kuisaidia wilaya hiyo, kwani wakati wa siasa umekwisha na kazi iliyombele yao wote ni kusaidia maendeleo ya wakazi wa wilaya hiyo.

"sitaki kusikia kuna miradi imekwama kwa ajili ya mambo ya siasa, chaguzi zimekwisha sasa tuchape kazi"alisema Ntibenda.

Awali wajumbe hao pia walipitisha mapendekezo ya kupeleka kwenye kikao cha kamati ya ushauri cha mkoa wa Arusha(RCC), kuomba barabara ya kutoka Ayasi-Endabash hadi Manyara kibaoni.

Mkuu wa wilaya hiyo, alisema barabara hiyo ni muhimu sana kwa maendeleo ya wilaya hiyo lakini halmashauri imeshindwa kuitengeneza kutokana na gharama kubwa kuhitajika ikiwepo ujenzi wa daraja.

Akizungumza katika kikao hicho, mbunge wa jimbo la Karatu, Mchungaji Israel Natse, aliwataka watendaji wa halmashauri ya Karatu kuacha kuwa vikwazo vya maendeleo.

Natse alisema hivi sasa wilaya hiyo, inakabiliwa na migogoro kadhaa  na kukwama kwa miradi ya maendeleo kutokana na baadhi ya watendaji wa halmashauri, wakiwepo watendaji wa vijiji kuwavuruga wananchi.

Kikao hicho, lichofanyika ukumbi ya maendeleo Karatu,pia kilishirikisha wawakilishi wa mashirika yasiyo ya kiserikali, vyama vya siasa, wakuu wa idara wa halmashauri ya karatu na viongozi katika ngazi mbali mbali za wilaya hiyo.

Imeandaliwa Fidelis Butahe, Dar na Juddy Ngonyani, Katavi, Burhani Yakub, Tanga na Mussa Juma, Arusha


No comments:

Post a Comment

sikiliza ngoma zinazo kamata kwa sasa

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...