Monday, December 24, 2012

MBOWE ASEMA HATUWEZI KUWA NA KATIBA MPYA ILIHALI TUNATUMIA SHERIA ZA ZAMANI, NINI MTAZAMO WAKO MSOMAJI WETU?


FREEMAN MBOWE, MWENYEKITI CHADEMA


WAKATI Rais Jakaya Kikwete akiwaapisha wajumbe wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Aprili 13 mwaka huu alionya kuwa mchakato wa kuandika Katiba Mpya usifanywe kwa kuegemea udini, ukabila, ubinafsi, siasa ama kulenga kuvunja Muungano.
Anasema maoni ya wananchi lazima yaheshimiwe hata kama hayataweza kuingizwa yote katika katiba hiyo, huku akiwataka wajumbe hao kuweka pembeni maslahi ya makundi wanayotoka kwa kuwa kazi wanayoifanya ni kwa maslahi ya taifa..
Tume hiyo ilianza kazi yake  ya miezi 18, Mei mosi mwaka huu, ambapo mpaka sasa imeshakusanya maoni katika mikoa takribani 15.
Mbali na kukusanya maoni ya wananchi na kutengeneza rasimu ya katiba, baadaye zitafuata  hatua mbili muhimu ambazo ni kuundwa kwa Bunge Maalumu la kuchambua rasimu hiyo, kisha wananchi kupiga kura ya maoni.
Tume hiyo ya Katiba leo ndio inamaliza kukusanya maoni ya Wananchi na kuanza kujipanga kwa taratibu nyingine za kumaliza kazi yake.
Pamoja na maelezo hayo ya Rais Kikwete watu wa kada mbalimbali likiwemo Jukwaa la Katiba Tanzania walipinga kwamba Katiba mpya haiwezi kupatikana Aprili 18, 2014 kama serikali inavyoeleza.
Wakipendekeza kwamba ili Katiba iweze kutumika ni lazima sheria nyingine zirekebishwe, zoezi ambalo huchukua miaka miwili.
Walisema kinachotakiwa kufanyika ni kurekebishwa kwa Ibara ya 98 ya Katiba ya sasa  katika vipengele vinavyohusiana na Tume ya Uchaguzi, ili uchaguzi wa mwaka 2015 uwe huru na wa haki, kuacha  mchakato wa kupatikana kwa Katiba mpya ukiendelea  kwa utaratibu mzuri.
Hoja hiyo ilinaonekana kuwagusa wengi na sasa,  Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Freeman Mbowe anasema jambo hilo linatakiwa kufanyiwa kazi haraka iwezekanavyo.
“Chadema tunaingiwa na hofu kwamba huenda Katiba mpya isiwe tayari kabla ya uchaguzi wa Serikali za mitaa mwaka 2014 na uchaguzi mkuu mwaka 2015” anasema Mbowe.
Anasema hakuna ulazima wa kupatikana kwa Katiba mpya katika kipindi hicho, badala yake mchakato huo uendelee lakini yafanyike marekebisho katika Sheria ya Uchaguzi ya mwaka 1985 ambayo ndani yake kuna Tume ya Uchaguzi (Nec) na daftari la kudumu la wapigakura.
“Kuna mambo yanatakiwa kufanyiwa kazi, kwanza ni kuwa na Tume huru ya Uchaguzi na mchakato wa kupata tume hii ufanyike bila kuathiri mchakato mzima wa kupata Katiba mpya.
“Tukienda katika chaguzi hizi mbili bila kubadili sheria nyingine zinazogusa maisha yetu ya kila siku ikiwemo hii ya uchaguzi ni wazi kuwa tutaingia katika machafuko, uchaguzi hauwezi kuwa huru na wa haki kama ukisimamiwa na muundo wa Nec hii inayoteuliwa na Rais” anasema Mbowe.
Anasema vyama vya upinzani haviwezi kujiandaa na Uchaguzi Mkuu ujao kwa sababu mpaka sasa havijui mfumo wa uchaguzi huo utakuwa wa namna gani.
“CCM wao wanajua kila kitu na ndio maana hawana wasiwasi, pia daftari la kupigia kura nalo ni tatizo kwa kuwa halijafanyiwa maboresho,” anasema Mbowe.
Anasema  licha ya mchakato wa Katiba kuendelea huku serikali ikieleza wazi kwamba Katiba itapatikana kabla ya mwaka 2015, wao hawaiamini kwa kuwa siasa ni mchezo mchafu.
“Hatuna sababu ya kukiamini chama tawala katika hili kwa sababu wanachokizungumza ni tofauti na wanachokifanya. Chama chochote makini lazima kianze kujipanga mapema lakini kwa utaratibu wa sasa hatuwezi kufanya hivyo,” anasema Mbowe na anaongeza;
“Tutafanya maandalizi kwa sheria ipi, hatujui Muungano utakuwa wa aina gani, lakini pia hatujui tutakuwa na Tume ya Uchaguzi ya aina gani na wala hatujui majimbo yatakuwa mangapi.”
Anasema kuwa kwa mara ya kwanza ilipotungwa sheria ya mabadiliko ya Katiba, chama hicho kiliipinga na kutaka ifanyiwe marekebisho katika sehemu tatu ambazo ni, muundo wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Bunge la Katiba na Kura ya Maoni.
“Pamoja na sheria hiyo kufanyiwa marekebisho lakini yaligusa sehemu moja tu kati ya hizo tatu,” anasema Mbowe.
Anasema hata kama Tume hiyo itamaliza kazi yake ya miezi 18, bado kuna ulazima wa mchakato wa kubadili sheria mbalimbali kuanza kufanywa.
“Chadema hatupingi mchakato wa Katiba Mpya, tume iendelee na zoezi lake lakini wakati huohuo ufanyike mchakato wa mabadiliko ya sheria mbalimbali ambazo zinaweza kutuletea matatizo katika uchaguzi,” anasema Mbowe.
Anasema wanaipinga sheria ya uchaguzi ya mwaka 1985 kwa kuwa ilitungwa wakati nchi ikiwa katika mfumo wa chama kimoja na hata Tume ya Uchaguzi  nayo iliundwa kwa mfumo huo huo.
“Ili nchi iwe na uchaguzi huru ni lazima vyama vyote vya siasa viwe na imani  na Tume ya Uchaguzi,  hata katika mechi ya mpira wa miguu lazima timu ziwe na imani na refa, tusikubali kuendelea kuwa na sheria mbovu kwa kigezo cha mchakato wa Katiba,” anasema Mbowe

No comments:

Post a Comment

sikiliza ngoma zinazo kamata kwa sasa

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...